KATIBU
Mkuu wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), Jerome Valcke,
anatarajiwa kuwasili nchini Mei Mosi mwaka huu ambako atafungua semina
ya mawasiliano itakayoshirikisha viongozi wa vyama wanachama wa Baraza
la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (Cecafa).
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Rais wa Shirikisho la Soka
Tanzania (TFF), Jamal Malinzi, alisema Valcke ambaye hii ni mara yake ya
kwanza kuja Tanzania, atafuatana na maofisa wengine saba wa FIFA.
Malinzi alisema semina hiyo iliyoandaliwa na FIFA, itafanyika kwa
siku mbili, ambapo vilevile Valcke atapata fursa ya kuzungumza na
waandishi wa habari wa ndani na wa kimataifa.
Rais huyo wa TFF, aliongeza kuwa washiriki wa semina hiyo ni marais,
makatibu wakuu na wakuu wa mawasiliano wa wanachama 12 wa Cecafa, ambao
ni Burundi, Djibouti, Eritrea, Ethiopia, Kenya, Rwanda, Somalia, Sudan,
Sudan Kusini, Tanzania na Uganda.
Naye Mwenyekiti wa Cecafa, Leodegar Tenga, ambaye alifuatana na
Katibu Mkuu wake, Nicholas Musonye, alimshukuru Rais wa TFF kwa kukubali
kuwa mwenyeji wa semina hiyo, kwani itasaidia katika maendeleo ya mpira
wa miguu katika ukanda huu.
freemedia
0 comments:
Post a Comment