pagead2.googlesyndication.com pagead2.googlesyndication.com

Kivuko Dar- Bagamoyo kuanza kazi karibuni

WAZIRI wa Ujenzi, Dk. John Magufuli, amesema kivuko kitakachofanya safari zake Dar es Salaam hadi Bagamoyo kinatarajiwa kuanza kutoa huduma kwa wananchi wiki tatu zijazo.
Dk. Magufuli alitoa kauli hiyo jana alipotembelea karakana ya kutengeneza na kukarabati meli na vivuko iliyopo Kurasini kwa ajili ya kuangalia maendeleo ya ukarabati wa kivuko cha Mv. Kigamboni yaliyoanza Agosti 14 mwaka huua.
Alisema mpaka sasa hivi wameshawasiliana na kampuni ya Denmark ambayo ndio imepewa zabuni ya kutengeneza kivuko hicho na wamewaambia wameshakidumbukiza majini tayari kwa safari ya kuja nchini.
Kwa mujibu wa Waziri huyo, Kivuko hicho kimepewa jina la MV Dar es Salaam na kitakuwa na uwezo wa kubeba watu zaidi ya 300 kinatarajiwa kupunguza foleni na adha ya usafiri kwa wakazi wa maeneo ya Tegeta, Bunju na Bagamoyo.
Akizungumzia kuhusu ukarabati wa kivuko cha MV Kigamboni, Dk. Magufuli alionekana kuridhika nao na kusema Jeshi la Wanamaji ambalo ndilo lilipewa zabuni ya kukikarabati limeonyesha uzalendo wa hali ya juu na kupunguza gharama.
Alisema kama kingepelekwa Mombasa zingetumika sh. milioni 600, lakini baada ya maamuzi ya kutengenezewa hapa nchini ni theluthi ya hela zilizotengwa ndizo zimetumika (sh milioni 200).
Kutokana na hali hiyo alilizawadia jeshi hilo ng’ombe wawili ambao alimkabidhi Mkuu wa Jeshi hilo, Brigedia Jenerali Regastian Laswai na kuongeza kuwa hali hiyo iwe fundisho kwa taasisi mbalimbali zinazopenda kupeleka vitu kukabatiwa nje ya nchi wakati tuna wataalam wa kutosha hapa nchini.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (Temesa), Mhandisi Marecellin Magesa, alisema pamoja na ukarabati huo bado nia ya Serikali ipo palepale ya kuongeza kivuko kingine kitakachosaidiana na vivuko vilivyopo na tayari sh bilioni 3.7 zimetengwa kwa ajili ya ununuzi wa kivuko hicho.

0 comments:

Post a Comment