pagead2.googlesyndication.com pagead2.googlesyndication.com

MASHINE ya kurushia matangazo ya BUNGE yaibiwa

MASHINE ya kurushia matangazo ya moja kwa moja na kuchanganya picha, imeibiwa ndani ya ukumbi wa jengo la Bunge katika mazingira ya kutatanisha, Tanzania Daima limebaini.
Mashine hiyo (Mixer), mali ya kituo cha Televisheni ya Star TV, imeibiwa ikiwa imehifadhiwa kwenye chumba maalum cha kurushia matangazo ya Televisheni na Radio za vituo mbalimbali baada ya kumalizika kwa Bunge Maalum la Katiba.
Ingawa thamani halisi ya mashine hiyo haijajulikana, lakini inaelezwa kuwa ina thamani kubwa ya mamilioni ya fedha na haipatikani nchini.
Mbali ya kuiba mashine hiyo, wajanja hao pia wameiba vingamuzi viwili vilivyokuwa vikitumika wakati wa kurusha matangazo ya moja kwa moja bungeni.
Uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima, umebaini kuwa mashine hiyo imeibiwa baada ya kumalizika kwa Bunge Maalum la Katiba na hakuna aliyenaswa wala kudaiwa kuhusika na wizi huo.
Habari za kiintelejinsia kutoka viwanja vya Bunge, zinasema kuwa tayari maofisa usalama wa Bunge wameanza kupitia picha za kamera za Bunge kusaka wezi hao.
Kutokana na kuibiwa kwa mashine hiyo, matangazo ya Televisheni ya Star TV na zingine zilizokuwa zikishirikiana kutumia kifaa hicho, yameathirika kwani hayako kwenye ubora unaotakikana.
Wizi huo umeibua maswali kutoka kwa baadhi ya wabunge na watumishi wa Bunge.
Baadhi ya wabunge walisema kwa namna jengo la Bunge lilivyo, hakuna uwezekano wa mtu kutoka nje ya mazingira ya Bunge kuja kuiba.
"Milango ya Bunge inaingia kwa kadi maalum na muda wote kamera zinamulika. Mwizi huyo ameingiaje na ametokaje bila kuonekana," alihoji mmoja wa watumishi wa Bunge.
Katibu wa Bunge, Thomas Kashilila, alikiri kuibiwa mashine hiyo anazo na Bunge imeanza kuzifanyia kazi.
Alisema anataka kupata maelezo ya kutosha kwa waandishi na wafanyakazi wa Star TV waliokuwa kazini wakati Bunge Maalum la Katiba lilipoahirishwa na namna walivyoamua kuiacha mashine hiyo iendelee kubaki ndani ya jengo la Bunge bila ofisi yake kuwa na taarifa.
“Kweli kuna hiyo mashine imeibiwa na jana nilipata barua rasmi ya kujulishwa kupotea kwa kifaa hicho. Nimetoa maelekezo kwa askari na wana usalama wa hapa kuanza kufuatilia na hatimaye tutalazimika kuangalia kwenye kamera kuanzia tarehe ya Bunge hilo lilipoahirishwa hadi sasa,” alisema Dk. Kashilila.

0 comments:

Post a Comment