pagead2.googlesyndication.com pagead2.googlesyndication.com

Aliyechoma watoto wake midomo jela miaka 5

Kamanda wa Polisi Morogoro, Faustine Shilogile.
Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Morogoro imemhukumu kifungo cha miaka mitano jela, Jaribu Juma (29), baada ya kupatikana na hatia ya kujeruhi na kufanya ukatili dhidi ya watoto.

Hukumu hiyo iliyotolewa huku mshtakiwa huyo akiwa hana ndugu hata mmoja aliyefika mahakamani hapo kushuhudia, imetolewa na Hakimu wa mahakama hiyo, Godfrey Isaya, baada ya kuridhishwa na ushahidi uliotolewa na mawakili wa Serikali, Sunday Hyera na Akisa Mhando.

Katika shtaka la kwanza la kujeruhi mtoto wa kwanza, mshtakiwa huyo alihukumiwa kwenda jela miaka minne, vivyo hivyo kwa kosa la pili, la kujeruhi mtoto wa pili, ambapo amehukumiwa adhabu kama hiyo ya miaka minne, huku kosa la tatu la ukatili dhidi ya mtoto akihukumiwa kulipa faini ya shilingi laki tatu, au kwenda jela miaka mitano, na kwa kosa la nne la ukatili dhidi ya mtoto mwingine, akipewa adhabu kama hiyo.
Hata hivyo, akifafanua hukumu hizo, Hakimu Isaya alisema kuwa mshtakiwa akiamua kutumikia adhabu zote kwa kifungo cha jela, adhabu hizo zote zitakwenda sambamba, hivyo atatumikia kifungo cha miaka mitano jela, na kwamba iwapo atalipa faini kwa kosa la tatu na la nne, basi atakwenda jela miaka minne.

Hakimu Isaya alisema mshtakiwa ana haki ya  kukata rufaa ndani ya siku 30 tangu hukumu kutolewa.

Kabla ya kutoa adhabu hizo, alisema mahakama imezingatia kuwa mshtakiwa ni baba wa watoto hao, na hilo ni kosa lake la kwanza, lakini ni baba aliyegeuka hatari kwa watoto wake na kujenga malezi na makuzi mabaya dhidi yao, tabia ambayo sio nzuri kwa wazazi na imekuwa ikijitokeza sana kwa jamii hivyo haipaswi kuachiwa.

Ilidaiwa kuwa mshtakiwa huyo alitenda kosa hilo Machi 13, mwaka huu, ambapo bila halali na kwa kujua kufanya hivyo ni kosa kisheria, aliwachoma moto midomo watoto wake wawili, Malick Jaribu (5) na Ibrahim Jaribu (10) baada ya kuwatuhumu kula karanga walizoachiwa kwaajili ya kuuza.

Kabla ya hukumu hiyo, mshtakiwa huyo alizua tafrani mahakamani, baada ya kugoma kuingia kwenye chumba cha mashtaka kusikiliza hukumu, ambapo alijiangusha chini na kujigalagaza, jambo lililowalazimu askari polisi kuingilia kati na kumnyanyua mshtakiwa huyo hadi ndani.

Aidha akijitetea kabla ya kutolewa hukumu hiyo, mshtakiwa huyo aliiomba mahakama kumuonea huruma kwa vile alikuwa ni baba wa familia, na tegemeo kwa watoto wake ambao amedumu nao kwa zaidi ya miaka minne sasa, na kuomba mahakama iwapo itabaini kurudia tena kosa kama hilo, impe adhabu kali ili iwe fundisho kwake na kwa wengine.

“Mheshimiwa hakimu, sikudhamiria kufanya hivi na ndio maana nimemua kukiri mbele hya baraza lako tukufu, lakini siwezi kusema mengi, mahakama itoe tu adhabu itakavyoona ili iwe fundisho kwangu na kwa wengine,”alisema mshtakiwa huyo ambaye awali aliomba mahakama kumuonea huruma kwa vile kosa hilo lilikuwa ni la kwanza.
 
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

Post a Comment