MENEJA wa Wafanyakazi wa Ndani ya Ndege wa Kampuni ya Fastjet,
Emma Donovan, alifikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala, Dar es
Salaam, kujibu shtaka linalomkabili la kutoa lugha ya matusi.
Emma (40) alipandishwa kizimbani jana na kusomewa shtaka hilo na
Wakili wa Serikali, Nassoro Katuga, mbele ya Hakimu Joyce Minde. Katuga
alidai Machi 19, mwaka huu, Emma alimtolea lugha ya matusi, Samson
Itinde, jambo ambalo ni kinyume cha sheria.
Emma alikana shtaka hilo, ambapo Katuga alidai upelelezi umekamilika na kuomba kupangiwa tarehe kwa usikilizwaji wa awali.
Hakimu Joyce alisema kuwa dhamana ya mshtakiwa iko wazi lakini kwa
kuzingatia vigezo vya dhamana vitakavyotolewa kwa kuwa mshtakiwa ni raia
wa kigeni.
Alitaja masharti ya dhamana kuwa mshtakiwa kuwasilisha hati yake ya
kusafiria au kutoa fedha taslim sh milioni tano na pia awe na wadhamini
wawili ambao ni Watanzania. Kutokana na uamuzi huo, kulijitokeza hali ya
sintofahamu mahakamani hapo hususan kutoka kwa wadhamini wawili ambao
ni Watanzania waliokuwa wanataka kumdhamini Emma.
Hilo lilisababishwa na wadhamini kushindwa kujibu kwa ufasaha baadhi
ya maswali waliyokuwa wanaulizwa na hakimu Joyce ikiwemo kutaja majina
ya mwenyekiti wa serikali yake ya mtaa na balozi wa nyumba kumi.
Hata hivyo, baada ya dakika 10, watu hao waliweza kupata majina ya
watu hao ambao awali walikuwa hawawafahamu majina yao kwa madai kuwa
huwa hawashindi majumbani kwao kwa muda mrefu.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Aprili 9 ili kupangwa tarehe ya kuanza kwa usikilizwaji wa awali.
chanzo Tanzania daima
|
|
0 comments:
Post a Comment