pagead2.googlesyndication.com pagead2.googlesyndication.com

Tutayajenga upya makaburi ya Sheikh Yahya na Sheikh Kassim - Serikali

makaburi

SERIKALI imesema itajenga makaburi ya mashekhe wawili maarufu, yaliyodaiwa kubomolewa na Mgambo wa jiji la Dar es Salaam katika operesheni ya usafi inayoendelea.
Katika operesheni hiyo, mgambo hao walidaiwa kuvunja makaburi ya Tambaza yaliyopo Upanga jijini Dar es Salaam, yakiwemo ya Shekhe Yahya Hussein na Shekhe Kassim bin Juma.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki alisema baada ya tukio hilo, walifuatilia na kubaini matingatinga yaliyotumika kubomoa makaburi hayakuwa yanayotumiwa na jiji.
“Awali familia za mashekhe hao zilieleza kutaka kugharamia ujenzi wa makaburi hayo, lakini sisi kama serikali tumeona tuyajenge na kuwaomba watuachie sisi,” alisema.

Alisema baada ya kuvunjwa kwa makaburi hayo, walichobaini ni kuwa kuna uwezekano jumuia ya wamiliki wa vibanda vilivyopo karibu na makaburi hayo, wanatengeneza njama ili kuzorotesha operesheni hiyo.
Alisema kuna watu wachochezi waliotumia makaburi ya viongozi hao ili familia zao zichukie serikali. Alisema pale kuna makaburi mengi, kwa nini yabomolewe ya viongozi pekee.
Aidha, Mkuu huyo wa mkoa alisema serikali haiwezi kujenga uzio katika makaburi hayo, kama familia za viongozi hao zilivyoomba, kwani wakifanya hivyo itabidi kujenga uzio makaburi yote mkoani humo, ambayo ni mengi.
“Ni vema kwa kutumia taasisi yao kujenga uzio, kwani serikali ikifanya hivyo itatumia gharama kubwa lakini mimi kama Sadiki nitaangalia namna ya kusaidia ombi hilo,” alisema.
Awali, mtoto wa marehemu Shekhe Yahya Hussein, Hassan Yahya Hussein alisema familia hizo mbili zimeumizwa na kitendo hicho na kuomba serikali iwasake na kuwachukulia hatua za kisheria waliohusika.
Alisema dawa ya kuepukana na matatizo kama hayo ni kujenga uzio katika makaburi hayo. Alisisitiza kuwa watajenga makaburi ya wazazi wao kwa gharama zao wenyewe.
Katika tukio hilo, familia inayomiliki eneo hilo la makaburi ililalamikia kitendo hicho na kusema kimefanyika usiku bila taarifa, na maeneo mengine hayahusiki na operesheni hiyo.
Msemaji wa familia hiyo, Msakala Tambaza alisema mgambo wa operesheni hiyo walipofika hapo, waliwaambia wamiliki wakae umbali wa mita 100 na dhahiri hao ndio walioharibu makaburi hayo.
Alitoa wito kwa serikali kuwalipa gharama za uharibifu wa makaburi na sehemu zilizobomolewa zisizohusika, walipwe gharama.

0 comments:

Post a Comment