pagead2.googlesyndication.com pagead2.googlesyndication.com

Mambo saba Varangati shoo ya Diamond Ujerumani haya hapa

SIKU chache baada ya kutolewa kwa taarifa ya kukamatwa kwa promota aliyempeleka msanii Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ nchini Ujerumani kwa ajili ya kufanya shoo aliyejulikana kwa jina la Awin Williams Akpomiemie, mwenye asili ya Kinigeria, nyuma ya sakata hili siri saba zimefichuka, Risasi Jumamosi lina ripoti kamili.
Mashabiki wenye gadhabu wakilizingira gari la Mbongo Fleva, 'Diamond Platinum' nchini Ujerumani.
SIRI YA KWANZA; KIBALI
Uchunguzi uliofanywa na mwanahabari wetu ulibaini kwamba katika sakata hilo lililojiri wiki mbili zilizopita, promota huyo aliwadanganya wamiliki wa Ukumbi wa Sindelfingen uliopo Mji wa Stuttgart, Ujerumani kuwa kutakuwa na mkutano wa Waafrika waishio nchini humo na baada ya hapo kutakuwa na pati ya kawaida. 

Ilisemekana kwamba wamiliki hao walitoa kibali kwa ajili ya mkutano hivyo walishtushwa kuona ukumbi umejaa na watu wanamsubiri Diamond kinyume na makubaliano.Kikizungumza kwa njia ya simu kutoka nchini humo, chanzo chetu kilidai kwamba ujanja alioutumia Awin kuwadanganya wamiliki wa ukumbi huo ndiyo chanzo cha fujo hiyo kwani alishindwa kuanza shoo mapema kwa kuwa wamiliki wa ukumbi hawakuwa tayari kwa jambo hilo.
Magari ya wagonjwa yakiwa tayari kuhudumia majeruhi eneo la tukio.
“Unajua siyo kila mtu anataka kuishi kwa shaka huku Ujerumani. Kila mtu anajua maisha ya Waafrika jinsi wanavyoishi, sasa uongo ungebainika mapema sidhani kama tungeishi kwa raha,” kilidai chanzo hicho. 

SIRI YA PILI; UTEKAJI
Habari kutoka nchini humo zilidai kwamba siri ya pili ni kwamba Diamond alikuwa atekwe kwani kulikuwa na waandaaji watatu wa mpango huo hivyo wawili walitaka kumteka msanii huyo ili akafanye shoo sehemu nyingine. 

“Mbali na Awin kulikuwa na jamaa wengine wawili ambao waliingilia mchakato mwishoni wakitaka waandae shoo hiyo lakini mwishoni walitofautiana ‘so’ walitaka waharibu ndiyo maana Diamond akachelewa ukumbini na vurugu zikatokea,” kilitonya chanzo chetu.
Mkali 'Diamond' akisepa kutoka eneo la tukio.
SIRI YA TATU; BIMA
Kikiendelea kutiririka, chanzo hicho kilidai kwamba ukiachana na uongo wa promota Awin iligundulika kwamba hakukuwa na bima ya kulinda usalama wa watu hasa endapo lingetokea tatizo kama lililotokea ambapo wengi walijeruhiwa. 

“Huku Ujerumani huwezi kufanya onesho lolote bila bima ya kulinda usalama kwenye shoo yako, sasa jamaa hakuwa nayo, kosa ambalo ni kubwa sana kwa sheria za Ujerumani,” alisema mtoa habari wetu. 

SIRI YA NNE; UKUMBI WA MIKUTANO
Kingine kilichogundulika ni kwamba hata ukumbi wenyewe ulikuwa wa mikutano na maonesho ya bidhaa na si wa kufanyia shoo za muziki kama alivyotaka kufanya yeye. 

“Ukumbi wa Sindelfingen, Stuttgart ni wa mikutano na maonyesho ya bidhaa, haujawahi kutumika kwa shoo kama ile ndiyo maana hata sisi tulishangaa iweje utumike kwa ajili ya shoo ya Diamond?” kilihoji chanzo chetu. 
Moja ya shoo aliyofanikiwa kufanya('Diamond') huko majuu.
SIRI YA TANO; HASARA MIL. 600
Chanzo hicho kilieleza kwamba baada ya uchunguzi wa polisi, ilibainika kwamba hasara iliyosababishwa na vurugu hizo inafikia euro 300,000 (zaidi ya Sh. milioni 600 za Kibongo).
“Hicho ndicho kiasi ambacho Awin anatakiwa kukilipa kwa wamiliki wa ukumbi kwani alisababisha loss (hasara) kubwa sana,” kilidai chanzo hicho. 

SIRI YA SITA; KESI
Licha ya promota huyo kufikishwa polisi kwenye Mji wa Stuttgart, suala lake lipo chini ya ofisi ya mji huyo ili sheria ichukue mkondo wake huku polisi wakisisitiza kwamba Diamond akitia mguu tu watamdaka.

“Hadi ninavyoongea na wewe polisi bado wanamuhoji Awin kutokana na tetesi kwamba anajihusisha na biashara tata lakini kuhusu fujo zile kesi yake iko chini ya ofisi ya Mji wa Stuttgart, inavyooneka hali iko vibaya sana kwa upande wake na Diamond kwani polisi wanakomaa kuwa akitimba tena watamkamata,” kilisema chanzo hicho.

'Diamond' akiwa na Meneja wake, Babu Tale.
SIRI YA SABA; KUTAFUTA ‘KIKI’
Uchunguzi mwingine wa gazeti hili ulibaini kwamba sakata la vurugu za Diamond nchini Ujerumani lilipangwa kwa makusudi ili kutafuta ‘kiki’ (umaarufu) na kuvuta hisia kupitia vyombo vya habari vya kimataifa ili kumpaisha zaidi. 

“Fuatilia majibu ya meneja wake, Babu Tale. Alisema kuwa vurugu zilikuwa mbaya lakini ni fagio kwa Diamond kimataifa. Kama siyo kutafuta kiki ni nini?” kilihoji chanzo makini Bongo na kuongeza:
“Nasikia anarudi Ujerumani kufanya shoo kubwa ya bure (Septemba 20). Wewe huoni hapo kulikuwa na mchezo?” 

DIAMOND ANASEMAJE?
Alipoulizwa Diamond kuhusiana na utayari wa yeye kurudi Ujerumani na yote yaliyotokea, hakutaka kufungukia zaidi ishu hiyo na kudai amejiaandaa vilivyo kufanya shoo ya bure Septemba 20 kama waandaaji walivyomtaka. 

TUMEFIKAJE HAPA
Agosti 30, mwaka huu zilitokea fujo kwenye Ukumbi wa Sindelfingen uliopo Mji wa Stuttgart, Ujerumani zilizosababishwa na Diamond ambaye alichelewa kupanda stejini hadi saa 10:00 alfajiri ambapo watu walivunja viti, vyombo vya muziki na vitu mbalimbali baada ya mashabiki kushikwa na hasira kwa kukosa  burudani ya shoo Diamond.

0 comments:

Post a Comment