pagead2.googlesyndication.com pagead2.googlesyndication.com

Madudu zaidi meno ya tembo

Balozi wa China, Lu Youqing akizungumza, jana mjini Arusha wakati wa Mkutano wa Kimataifa wa Kudhibiti Ujangili. Wengine ni Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu (katikati) na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, James Lembeli Picha na Filbert Rweyemamu 

Dar es Salaam. Wakati maofisa wa Serikali za Tanzania na China wakipuuza tuhuma zinazohusisha ziara ya Rais wa China, Xi Jinping na utoroshaji wa meno ya tembo, ripoti hiyo imeanika madudu mengi ikionyesha jinsi nyara hizo zinavyotoroshwa nchini.
Juzi taasisi iitwayo Environmental Investigation Agency (Wakala wa Uchunguzi wa Mazingira– EIA) ilitoa hadharani ripoti ambayo inataja maofisa na wanausalama wa China kwamba walitumia fursa ya kidiplomasia kusafirisha meno ya tembo kwa ndege ya Rais Jinping ambaye alitembelea Tanzania Machi 2013.
Ikulu ya Dar es Salaam na Ofisi ya Mambo ya Nje ya China kwa nyakati tofauti zilisema taarifa hizi siyo za kweli na jana Serikali ya Tanzania kupitia kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, ilitoa taarifa bungeni na kuziita taarifa hizo kuwa ni za “kupikwa”.
Wakati hayo yakiendelea, ripoti hiyo ya EIA iliyopewa jina la Vanishing Point: Criminality, Corruption and Devastation of Tanzania’s Elephants (Hatua ya kutoweka: Uhalifu, Rushwa na Kuangamizwa kwa tembo wa Tanzania), inafichua madudu zaidi yanayoweka bayana jinsi uhalifu wa utoroshaji wa meno ya tembo unavyofanyika.
Ripoti hiyo inalitaja pori la akiba la Selous kuwa kituo cha mauaji ya tembo, kwani matukio ya ujangili hupangwa katika vijiji vinavyozunguka hifadhi hiyo, kisha kutekelezwa kwa msaada wa polisi na baadhi ya wananchi.
Inavitaja vijiji vilivyopo katika maeneo ya Mloka, Tunduru, Namtumbo, Liwale na Kilwa ambako wafanyabiashara wadogo kutoka Dar es Salaam hukodishwa silaha na wawindaji, kisha kuingia katika hifadhi hiyo na kufanya uhalifu.
“Wakati mwingine wawindaji kutoka nje ya eneo hilo hutumiwa na baadhi ya maofisa kutoka serikalini,” inasomeka sehemu ya ripoti hiyo.
Katika tukio la aina yake, ripoti hiyo imeeleza tukio la katikati ya mwaka huu ambapo kundi la wawindaji kutoka Arusha lilitumwa na maofisa wa polisi waliokuwa Mloka na kuingia katika hifadhi hiyo kwa ajili ya kuwinda.
Inadaiwa kuwa maofisa hao wa polisi walitoa silaha kwa kundi hilo la wawindaji na baada tu ya mauaji ya tembo wapatao watano walichukua meno kutoka kwa wawindaji.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, tembo akishauawa, meno yake hukatwa kisha kufukiwa hadi pale mnunuzi anapowasili ambapo hufukuliwa na kupewa.
EIA katika ripoti hiyo inabainisha kuwa meno mengi ya tembo kutoka Selous husafirishwa kwenda Dar es Salaam, ama kwa kutumia barabara kwa maana ya magari ambayo yametengezwa maalumu kwa ajili ya kazi hiyo, au kwa kupitia majini wakitumia mitumbwi ya asili.
“Wakati mwingine pikipiki hutumika kupitia njia za vichakani kukusanya meno hayo kule ambako zimefichwa hadi kufikia barabara kuu,” inasema sehemu ya ripoti hiyo. Kutoka kwenye njia kuu husafirishwa kwa magari binafsi ambayo yanakuwa sehemu maalumu kwa ajili ya kuficha pembe hizo au kupitia mabasi ambayo husafirisha meno ya tembo zaidi kuliko abiria kutokana na malipo makubwa ambayo hutolewa kwa kazi hiyo.
Ripoti hiyo inaongeza kuwa: “Kwa kawaida meno ya tembo mabichi yanapofikishwa jijini Dar es Salaam kutoka Kusini huwekwa katika mafungu madogo na kuhifadhiwa katika baadhi ya maeneo kwenye vitongoji vya jiji hilo. Pindi anapotokea mteja anahitaji kununua hukusanywa na kuuziwa”.
Inaelezwa kuwa kawaida hifadhi hizo huwa katika maeneo ya viwanda kama vile Chang’ombe karibu na bandari, lakini pia wakati mwingine katika viwanja vilivyopo mbali na makazi ya watu.
Selous hatarini
Kutokana na hali hiyo, ripoti hiyo inasema Hifadhi ya Selous ipo katika hatari ya kupoteza hadhi yake kutokana na kukithiri kwa matukio ya ujangili, huku Serikali ikionekana kwamba haijali.
Ripoti hiyo inadai kuwa hifadhi kongwe yenye maeneo makubwa yapatayo kilomita za mraba 50,000 haina ulinzi wa kutosha hali inayotoa mianya kwa makundi ya uhalifu wa wanyamapori kufanya vitendo hivyo.
EIA inasema idadi ya tembo katika Hifadhi ya Selous imeshuka kutoka 70,406 mwaka 2006 hadi kufikia 13,084 mwaka 2013. Hiyo ikimaanisha kwamba idadi ya tembo 57,322 wameuawa katika kipindi cha miaka saba.
Mauaji hayo yamethibitishwa kwa kipimo cha vinasaba (DNA) na kubainisha kuwa asilimia kubwa ya mauaji ya tembo yanahusishwa na ukataji wa pembe za ndovu.
Kwa mujibu wa EIA mwaka 2000 tayari kulikuwa na ishara za wazi zilizoonyesha kuwapo kwa mauaji ya tembo na kwamba baadhi ya vyombo vya habari viliripoti juu ya hali hiyo hasa baada ya mizoga ya tembo kuonekana ikiwa imezagaa katika hifadhi ya Selous. “Lakini, mkurugenzi wa wanyamapori alipoulizwa kuhusiana na hali hilo, alisema kuwa matukio ya ujangili yapo chini,” inasomeka sehemu ya ripoti hiyo yenye kurasa 36.
Inaendelea kueleza kuwa, mwaka 2010, EIA walitembelea eneo la Selous na kufanya mahojiano na wanakijiji ambao walifichua siri juu ya maeneo yanayotumika kufanyia biashara haramu ya meno ya tembo.
Njia za magendo zinazotumika kusafirisha meno hayo zinawahusisha polisi na askari wanyamapori ambao taarifa hiyo inawataja kwamba wao ndio waliopaswa kuwa mstari wa mbele kulinda hifadhi hizo, hali inayoifanya EIA kuitupia lawama Serikali ya Tanzania.
“Licha ya ishara hizi za wazi, Serikali ya Tanzania imeshindwa kupambana na ujangili katika Hifadhi za Selous. Zaidi ya tembo 25,000 waliuawa kati ya mwaka 2010 na mwaka 2013. Sababu kuu iliyosababisha vifo vya tembo hao ni ujangili.
“Mwaka 2011, theluthi mbili ya mizoga ilionekana katika Hifadhi ya Selous. Sababu inayochangia ni ukosefu wa rasilimali kwa ajili ya kulinda hifadhi kwa umakini,” inasomeka sehemu ripoti hiyo.

0 comments:

Post a Comment