pagead2.googlesyndication.com pagead2.googlesyndication.com

Izzuddin Qassam: Mapambano bado yanaendelea

Izzuddin Qassam: Mapambano bado yanaendelea
Kamanda Mkuu wa Brigedi ya Izzuddin Qassam tawi la kijeshi la Harakati ya Muqawama wa Kiislamu wa Palestina Hamas amesema kuwa, ni muhali kupatikana makubaliano ya usitishaji vita, bila ya kukomeshwa mashambulio ya majeshi ya utawala wa Israel na kuondolewa mzingiro wa Ukanda wa Gaza. Kamanda Muhammad Dhwayf amesisitiza kuwa, usitishaji vita hautakuwa na maana kama hayatakomeshwa mashambulizi ya kijeshi ya Israel huko Ghaza na kuondoshwa kikamilifu mzingiro unaowakabili wananchi wa Palestina katika eneo hilo kwa miaka saba sasa. Wakati huohuo, Msemaji wa Jeshi la Israel amesema kuwa, jeshi la utawala huo limewaita askari wengine elfu kumi na sita wa kikosi cha dhiba kwa ajili ya kushiriki kwenye operesheni za Gaza. Msemaji wa Jeshi la Israel ameongeza kuwa, kuongezwa wanajeshi hao wa dhiba, kutaifanya idadi ya askari wa Israel walioko katika mpaka wa Gaza kufikia  elfu themanini na sita. Hayo yanajiri katika hali ambayo, Kanali ya 2 ya Televisheni ya Israel imetangaza kuwa, zaidi ya askari 140 wa Israel wanapatiwa matibabu hospitalini, ambapo 16 kati yao wako mahututi. Utawala wa Israel umekuwa ukificha kutangaza idadi ya wanajeshi wanaouawa au kujeruhiwa, kwa shabaha ya kukwepa kuwavunja moto wanajeshi wa utawala huo. Kwa upande mwingine, jeshi la Israel limefanya mashambulizi zaidi ya elfu arobaini ya ardhini, angani, na baharini dhidi ya Gaza tokea ulipoanzisha vita dhidi ya eneo hilo yapata zaidi ya wiki tatu zilizopita. Taarifa zinasema kuwa, jeshi la Israel limeharibu zaidi ya misikiti 70, huko Ghaza. Inafaa kuashiria hapa kuwa, mmoja katiya maafisa waandamizi wa jeshi la Marekani amesema kuwa, wiki iliyopita Washington ililikabidhi jeshi la Israel ghala zake za silaha za makombora, magari ya kijeshi, zana na mizinga kwa ajili ya kuendesha operesheni za kijeshi huko Gaza. 

0 comments:

Post a Comment