pagead2.googlesyndication.com pagead2.googlesyndication.com

Tangazo la Shirika la Umeme Zanzibar

SHIRIKA LA UMEME ZANZIBAR
Tarehe 15/02/2014
TAARIFA KWA UMMA KUPITIA VYOMBO VYA HABARI JUU YA HALI YA KUKATIKA UMEME ZANZIBAR
Tangu kuanzia mwishoni mwa mwezi Januari, 2014, Zanzibar imeshuhudia mabadiliko ya hali ya hewa. Mabadiliko ambayo yamekuwa yakiathiri sana miundo mbinu ya umeme katika visiwa vya Unguja na Pemba.
Hali ya upatikanaji umeme Zanzibar kwa sasa tokea kuanza kwa mwezi huu wa pili imekuwa siyo ya kuridhisha katika baadhi ya maeneo. Umekuwepo ukatikaji wa umeme mara kwa mara hususan katika njia zinazosafirisha umeme kuelekea mashamba kama vile njia ya Kaskazini, Kusini, Fumba na baadhi ya maeneo ya mjini.
Kuanguka kwa nguzo za umeme, kupasuka kwa vikombe (pin insulators) katika njia za kusafirisha umeme pamoja na uchakavu wa miundo mbinu vimekuwa ni sababu kubwa inayopelekea kukatika kwa umeme mara kwa mara hivi sasa.
Mvua zinazoendelea kunyesha na upepo unaovuma kwa kasi hupelekea kuanguka kwa nguzo na hatimae umeme kukosekana. Vilevile, radi zinazopiga huathiri kwa kuunguza vifaa vilivyo katika miundo mbinu ya umeme na hatimae pia umeme hukosekana.
Hali hii vile vile inapotokea kwa upande wa Tanzania Bara, husababisha ongezeko la kasi ya umeme (over voltage) katika njia inayosafirisha umeme kuleta Zanzibar na hupelekea kisiwa chote kukosa umeme kama ilivyotokea kwa siku ya Ijumaa ya tarehe 14/02/2014 asubuhi na usiku.
Katika kushughulikia usalama wa miundo mbinu ya umeme, kama vile ubadilishaji wa nguzo mbovu, kila siku za Alhamisi na Jumamosi, Shirika la Umeme (ZECO) linafanya juhudi za kubadilisha nguzo hizo ili kumaliza kasoro hiyo katika njia zake za kusafirishia umeme. Vilevile, juhudi za Shirika zimeelekezwa katika kuzifanyia matengenezo ya mara kwa mara njia zake za ndani zinazosafirisha umeme ili kuondokana na kero za kukosekana kwa umeme.
Mwisho, Shirika linaomba radhi kwa wananchi na wateja wake ambao wamekuwa wakipata usumbufu kutokana na tatizo la kukatika kwa umeme mara kwa mara.
Aidha, Shirika linahitaji ushirikiano kutoka kwa wateja na wananchi kwa ujumla kwa kulipatia taarifa Shirika endapo hali yoyote isiyo salama katika miundo mbinu ya umeme itajitokeza. Taarifa hizo zitatoa fursa kwa Shirika kuweza kuchukuwa hatua za kuepesha madhara au kero zinazoweza kutokea. Vile vile Shirika linatoa wito kwa watu wote kuacha kusogelea au kugusa nyaya za umeme zilizoanguka chini kwani ni hatari mno.
Kwa kutoa taarifa, tafadhali piga simu nambari 0242 230 232

0 comments:

Post a Comment