pagead2.googlesyndication.com pagead2.googlesyndication.com

Marufuku watoto kuogelea Coco Beach siku za pasaka - Polisi

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, limepiga marufuku watoto wadogo kwenda kuogelea kipindi cha Sikukuu ya Pasaka.
Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, alisema jana kuwa watoto wadogo hawataruhusiwa kuogelea mpaka kuwe na mlinzi ambaye atakuwa nao na anayejua kuogelea.
Alisema hali hiyo inatokana na mvua zinazoendelea kunyesha, hivyo bahari haitakuwa shwari.
“Kutokana na hali ya hewa ilivyo pamoja na sababu za kiusalama na matishio mbalimbali katika ukanda wa Afrika ya Mashariki, tumepiga marufuku watoto kuogelea na  kwenda disco toto katika kumbi mbalimbali kwa kuwa sifa za kumbi kizo hazikidhi viwango vya kiusalama,” alisema.
Aliongeza kuwa madereva wanatakiwa kuzingatia sheria za usalama barabarani ikiwa ni pamoja na kutoendesha vyombo vya moto kwa mwendo kasi, wasiwe walevi, magari au pikipiki zenye sauti kali/zenye kuleta mshtuko nazo ni marufuku.
Pia Kamanda Kova aliwataka wananchi wanapoona dalili zozote au maandalizi ya uvunjifu wa amani watoe taarifa mapema iwezekanavyo katika vituo vya karibu, ili hatua zichukuliwe haraka.
“Mtu yeyote atakayeonekana au atakayesababisha uvunjifu wa amani au madhara yoyote atawekwa ndani mpaka sikukuu iishe na atapelekwa mahakamani,” alisema.
Alisema jeshi hilo limejipanga vema, kwani  kuanzia saa 10 jioni kutakuwa na doria itakayofanywa angani kwa kutumia helikopta ya Jeshi la Polisi kuangalia hali ya usalama katika Jiji la Dar es Salaam, pia kutakuwa na doria za pikipiki na doria za miguu katika barabara zote muhimu.
Pia alisema vikosi vyote vikihusisha askari wa vyeo vyote vitakuwa barabarani saa sita kabla ya mkesha wa Pasaka pamoja na kutumia Kikosi cha FFU kikijumuisha askari wa magari ya washawasha, askari wa Mbwa na Farasi.
“Wananchi wanashauriwa kusherehekea Sikukuu ya Pasaka katika ngazi ya familia au kukusanyika katika mitaa kwa amani,” alisema Kova.

0 comments:

Post a Comment