pagead2.googlesyndication.com pagead2.googlesyndication.com

Tuzo aliyopewa JK aitoa kwa Watanzania

JK atoa tuzo kwa Watanzania RAIS Jakaya Kikwete ametoa tuzo ya Kiongozi Bora wa Maendeleo Afrika aliyoipata hivi karibuni kwa ajili ya Watanzania wote ili kuonyesha heshima kwao.
Alisema Watanzania wamechangia katika maendeleo yaliyomwezesha kutunukiwa tuzo hiyo ya kimataifa, hivyo ni zawadi kwa ajili ya Watanzania wote popote walipo.
“Napokea tuzo hii kwa niaba ya Watanzania wote… naitoa kwa Watanzania kwa sababu hata kama nimekuwa kiongozi ukweli ni kwamba mafanikio na maendeleo yote yaliyopatikana na kuipata tuzo hii yametokana na juhudi zetu za pamoja,” alisema.
Rais Kikwete alipokea tuzo ya Kiongozi Bora wa Maendeleo Afrika mwaka 2013 kwa kuwa kiongozi wa utumishi bora kwa umma Afrika na aliyetoa mchango mkubwa zaidi kwa maendeleo ya uchumi wa wananchi wake kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, kwenye halfa iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam jana asubuhi.
Waziri Membe alipokea tuzo hiyo kwa niaba ya Rais Kikwete katika sherehe zilizofanyika kwenye Hoteli ya St. Regis jijini Washington, Marekani usiku wa Aprili 9, mwaka 2014.
Tuzo hiyo hutolewa kila mwaka na jarida maarufu la kimataifa la African Leadership Magazine kwa kiongozi wa Afrika aliyetoa mchango mkubwa zaidi wa maendeleo kiuchumi kwa wananchi wake na Rais Kikwete alikuwa rais wa tatu Afrika kupokea tuzo hiyo.
Tuzo hiyo iliwahi kutolewa pia kwa marais wa Sierra leone na Liberia kabla ya kupewa Rais Kikwete.
Akipokea tuzo hiyo mbele ya waandishi wa habari, Rais Kikwete alisema ina maana kuwa dunia inaona, inatambua na inathamini kazi inayofanywa na Watanzania katika jitihada za kujiletea maendeleo.
Tuzo hiyo ilikabidhiwa kwa Waziri Membe na Balozi wa Nigeria nchini Marekani, Profesa Ade Adefuye, kwa niaba ya Rais Goodluck Jonathan ambaye awali alipangwa kukabidhi tuzo hiyo kwa Rais Kikwete.
Profesa Adefuye alisema: “Kwa niaba ya Nigeria na kwa niaba ya Bara la Afrika nawasilisha kwenu Mwafrika wa wakati huu, mtoto maarufu wa Tanzania na mtoto maarufu wa Afrika, Rais Jakaya Kikwete.”

0 comments:

Post a Comment