pagead2.googlesyndication.com pagead2.googlesyndication.com

Odinga akwaa kisiki tena

Waziri Mkuu, Raila Odinga
Nairobi.Mahakama ya Juu ya Kenya imemthibitisha Uhuru Kenyetta kuwa Rais halali mteule wa nchi hiyo pamoja na mgombea mwenza wake, William Ruto.

Mahakama hiyo iliwathibitisha Kenyatta na Ruto jana katika uamuzi wa kesi ya kupinga matokeo uliowapa ushindi katika uchaguzi mkuu uliofanyika Machi 4, 2013, iliyofunguliwa na mpinzani wao mkuu katika kinyang’anyiro hicho, Waziri Mkuu, Raila Odinga.

Odinga katika kesi hiyo aliituhumu Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka ya nchi hiyo kuwa ilihujumu matokeo ya uchaguzi ili kumpa ushindi, Kenyatta.Hata hivyo, katika uamuzi wake jana Mahakama hiyo ilisema kwamba Kenyatta na Ruto walichaguliwa kihalali katika uchaguzi huo mkuu.

Vilevile, Jaji Mkuu wa Mahakama hiyo, Dk Willy Mutunga alisema kwamba uchaguzi ulikuwa wa haki na huru, kwa sababu katiba na sheria zilifuatwa, hivyo Mahakama imempitisha Rais huyo Mteule kuwa Rais wa Kenya.

Akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya kutolewa hukumu hiyo, Odinga alisema kwamba amekubaliana na uamuzi wa Mahakama kama alivyoahidi.
‘’Naitakia kila la kheri Serikali ya Uhuru Kenyatta, kwani hakuna ushindani usiokuwa na mshindi,’’alisema .

Aliwaasa Wakenya wakae kwa amani na kuheshimu Serikali mpya inayokuja baada ya kumalizika kwa kesi za uchaguzi katika Mahakama ya juu.
“Nilisema kwamba nitakubali uamuzi wa Mahakama ya juu kwani ikiwa sikajubaliana na uamuzi huo nitakuwa nimevunja sheria,’’alisema Odinga.

Hata hivyo Odinga alisema licha ya Mahakama hiyo kuacha kutendea haki baadhi ya vipengele vya kesi hiyo amekubali uamuzi huo.
Kutokana na ushindi huo, Kenyatta kutoka Muungano wa Jubilee sasa anafahamika kuwa ndiye Rais Mteule halali wa Kenya atakayeapishwa Aprili 9 mwaka huu.

Kesi hiyo ilifunguliwa na Raila Odinga wa Muungano wa Cord baada ya kumalizika kwa uchaguzi mkuu uliofanyika mapema mwezi huu.
Katika uchaguzi huo matokeo yalionyesha kuwa Uhuru alishinda kwa asilimia 50.07 huku Raila akipata asilimia 43.28 ya kura.

Uchaguzi huo ni wa kwanza tangu kufanyika uchaguzi uliokumbwa na ghasia mwaka 2007 na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 1,000.
Kenyatta na mgombea mwenza wake, Ruto, wanakabiliwa na kesi katika Mahakama ya Kimataifa Makosa ya Jinai wakituhumiwa kwa kuchochea vurugu zilizotokea mwaka 2007.

Kura kuhesabiwa tena
Machi 25, Mahakama ya Juu ya Kenya iliagiza kuchunguzwa kwa fomu 34 za matokeo ya uchaguzi wa rais kutoka katika vituo vyote 34,400, vya kupigia kura vilivyotumika katika uchaguzi mkuu wa nchi hiyo uliofanyika Machi 4, mwaka huu.

Kadhalika Mahakama hiyo iliagiza kuhesabiwa upya kwa kura za urais katika vituo 22 kati ya 33,000 vilivyolalamikiwa na aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Cord, Odinga.
Odinga alidai kuwa vituo hivyo 22 kura zilizopigwa zinazidi idadi ya wapiga kura walioandikishwa.


Ukiachilia mbali kesi iliyofunguliwa na Odinga kupinga Kenyatta kutangazwa mshindi wa uchaguzi huo wa tano tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi nchini Kenya, kuna kesi nyingine ambayo ilifunguliwa na Muungano wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali, `The African Centre for Open Governance’ (Africog). Katika kesi hiyo, Africog ilihoji uhalali wa uchaguzi huo.

Kesi ya tatu ilifunguliwa na wajumbe wa timu ya kampeni ya Kenyatta, Wanaharakati kutoka katika mitandao ya kijamii, Dennis Itumbi na Moses Kuria wanaopinga uamuzi wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka ya kujumuisha kura zilizoharibika wakati wa kujumlisha kura za wagombea urais.

Katika uamuzi wake, Mahakama iliamua kwamba kesi zote tatu zitaunganishwa kuwa moja mbali na ile iliyowasilishwa na Odinga .



Ombi la mashirika latupwa
Awali Mahakama ya Juu ilitupilia mbali ombi la muungano wa mashirika yasiyo ya kiserikali lililoitaka Mahakama hiyo iiamuru Tume ya Uchaguzi kufikisha mahakamani hapo nyaraka zote zilizotumika wakati wa uchaguzi huo.
Kadhalika Mahakama hiyo ilitupilia mbali hati ya kiapo yenye kurasa 839 iliyowasilishwa na Cord ikidai kuwa kura katika majimbo 120 zilikuwa haziwiani na idadi ya wapiga kura hivyo kuitaka Mahakama hiyo iitishe uchunguzi wa kina wa daftari la wapigakura ukioanishwa na kura zilizopigwa.

Maandamano
Juzi Jeshi la Polisi nchini Kenya lilifanikiwa kuzuia maandamano yaliyopangwa kufanyika nje ya Mahakama ya Juu mjini Nairobi wakati kesi hiyo ikiendelea.Waandamanaji hao walidaiwa kuwa ni kambi ya Waziri Mkuu, Odinga walikuwa wakipinga mwenendo wa kesi hiyo ulivyokuwa ukiendelea mahakamani hapo.

chanzo mwananchi

0 comments:

Post a Comment